SERIKALI YAENDELEA KUIMARISHA MATUMIZI YA MFUMO WA PD-MIS KWA WATENDAJI ARUSHA
Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com

Na mwandishi wetu, Arusha.
Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu imeendelea kuimarisha huduma kwa watu wenye ulemavu kwa kutoa mafunzo ya matumizi ya Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji na Usimamizi wa Taarifa za Watu Wenye Ulemavu (PD-MIS) kwa watendaji wa mkoa wa Arusha.
Mafunzo hayo yametolewa na Wataalamu kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kwenda kwa Maafisa Ustawi wa Jamii pamoja na Maafisa TEHAMA kutoka halmashauri mbalimbali za Mkoa wa Arusha kwa lengo la kuwajengea uwezo na kuimarisha matumizi ya mfumo huo katika ukusanyaji, uhifadhi na usimamizi wa taarifa sahihi za watu wenye ulemavu yamefanyika 28 April 2026, katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Afisa kutoka Kitengo cha Huduma kwa Watu Wenye Ulemavu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Bw. Gerold Komba, alisema Serikali inaendelea kuhakikisha inaendelea kuweka mipango yake vizuri katika kuhakikisha kwamba kundi hili la watu wenye ulemavu linahudumiwa ipasavyo nchi nzima.
Alisema Mfumo huu wa PD-MIS kwasasa umeshasambazwa katika mikoa mbalimbali ambapo kwasasa mikoa yote ya Kanda ya ziwa, Magharibi na Kanda ya Kusini imeshafikiwa na Mfumo huu, na kwasasa Mfumo umeanza kanda ya kaskazini katika mkoa wa Arusha.
Kwa upande wake Afisa Ustawi wa jamii Mkoa wa Arusha Bw. Dennis Mgie ameishukuru Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa kuandaa mafunzo haya kwani kupitia Mfumo huu takwimu za mkoa zinakua zenye ufanisi lakini pia zitawaongoza kwenye kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu.
"Takwimu hizi zitatusaidia kuweza kuwaunganisha watu wenye ulemavu na huduma na fursa mbalimbali ambazo serikali inawezesha watu wenye ulemavu ambao tutawatambua kwa hali zao na kazi zao kupitia mfumo huu",amesema Bw. Mgie.











No comments: