MADIWANI ILEMELA WAPITISHA BAJETI YA BILIONI 101.74
Yaliyomo humu (Habari, Matangazo na Maoni) si msimamo wa BMG Media. Mawasiliano +255 757 432 694 ama ripotabmg@gmail.com
Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza, Sarah Ng'wani akizungumza kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo, kilichoketi Jumatatu Januari 26, 2026.
Na Hellen Mtereko, Mwanza
Baraza la Madiwani Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza limepokea, kujadili na kupitisha mapendekezo ya mpango wa bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 yenye jumla ya kiasi cha shilingi Bilioni 101.74 za Tanzania.
Baraza hilo limejadili na kupitisha makadirio hayo ya bajeti Jumatatu Januari 26, 2026.
Akizungumza baada ya kupitishwa kwa bajeti hiyo, Mstahiki Meyaa wa Manispaa ya Ilemela, Sarah Ng'wani aliwaomba wataalamu na madiwani kushirikiana kwa pamoja katika kufikisha elimu kwa wananchi hatua itakayosaidia kurahisisha ukusanyaji wa mapato.
"Rai yangu kwa mnaoenda kukusanya mapato, niwaombe sana mkusanye kwa njia rafiki, msitumie nguvu bali muwe na njia sahihi ya kuwashawishi wafanyabiashara ikiwemo kutoa elimu" alisema Ng'wani.
Wakizungumzia bajeti hiyo, baadhi ya madiwani walieleza namna ilivyogusa changamoto za wananchi katika Kata zote za Manispaa ya Ilemela ikiwemo elimu.
Fredy Kisaka ambaye ni diwani wa Kata ya Nyasaka na pia Mjumbe wa Kamati ya Huduma, aliwaomba madiwani wenzake kuanzisha vyanzo vipya vya mapato ili waweze kushiriki kwa pamoja katika kuendeleza na kukuza mapato ya Halmashauri.
Naye diwani wa viti maalum, Sara Manyama alisema kazi yao ni kuendelea kuhamasisha upatikanaji wa mapato ili waweze kupata fedha za kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo.
Awali akiwasilisha mpango wa bajeti hiyo, Mchumi wa Manispaa ya Ilemela, Herbert Bilia alisema miongoni mwa vipaumbele vilivyopo kwenye bajeti hiyo ni kuhakikisha huduma bora za kijamii zinatolewa kwa wananchi na pia kuboresha miundombinu.
Mstahiki Meya Manispaa ya Ilemela, Sarah Ng'wani (kulia) akiwa na Naibu Meya wa Manispaa ya Ilemela, Kuluthum Abdallah (kushoto) kwenye kikao cha Baraza la Madiwani.



No comments: